Kiungo mshambuliaji wa Simba, Keletso Makgalwa, amewaomba mashabiki wa timu hiyo kuwa na subira naye akieleza kuwa bado anaendelea kuzoea mazingira ya soka la Tanzania na ushindani uliopo ndani ya kikosi.
Makgalwa alijiunga na Simba katika dirisha lililopita la usajili akitokea Sekhukhune United ya Afrika Kusini, akiwa miongoni mwa wachezaji waliosababisha gumzo kubwa wakati wa dirisha hilo.
Hata hivyo, tangu kuwasili kwake Simba, Makgalwa bado hajafikia kiwango ambacho mashabiki wengi walitarajia, jambo ambalo limezua maswali kuhusu uwezo wake wa kuonyesha makali yake akiwa kwenye kikosi hicho.
Akizungumzia hali hiyo, Makgalwa amesema sababu kubwa ni ugeni wa ligi, akisisitiza kwamba anahitaji muda zaidi ili kuzoea ushindani na mazingira mapya.
Bado anaizoea ligi
Makgalwa amesema anaamini ni suala la muda kabla ya kuanza kuonyesha uwezo wake kikamilifu, huku akisisitiza kuwa jambo la muhimu zaidi kwake kwa sasa ni mafanikio ya timu badala ya kutafuta mafanikio binafsi.
“Nafikiri jambo muhimu ni timu kwanza na sio mtu binafsi, mimi bado najaribu kuizoea ligi. Ni jambo la muda tu.”
Kauli yake inaashiria kuwa mchezaji Makgalwa anaamini ana uwezo wa kufanya makubwa akiwa Simba, licha ya kutopata nafasi kubwa kama ambavyo baadhi ya mashabiki walivyotarajia.
Ushindani mkubwa ndani ya kikosi
Mbali na changamoto ya kuzoea ligi, Makgalwa amekiri kuwa ushindani ndani ya kikosi cha Simba kwa sasa ni mkubwa, hasa katika nafasi anayocheza.
Amesema wachezaji wanaopata nafasi zaidi chini ya Kocha Mkuu Steve Barker wanafanya vizuri, jambo ambalo linamlazimisha yeye kuendelea kujifunza na kusubiri nafasi yake.
Makgalwa amewataja Libasse Gueye na Anicet Oura kuwa miongoni mwa wachezaji anaoshindana nao katika nafasi hiyo.
“Simba ina wachezaji bora sana wanaocheza kwenye nafasi yangu, kuna Libasse na Oura, najifunza vingi kutoka kwao,” alisema
Kocha Mkuu wa Simba Steve Barker ameendelea kumpa nafasi winga huyo mahiri akimuanzisha kwenye mchezo uliopita wa ligi ya mabingwa dhidi ya Mighty Wonderers akichukua nafasi ya Gueye ambaye alikuwa akitumikia adhabu ya kadi nyekundu.
Gueye anatarajiwa kurejea kikosini kwenye mchezo wa marudiano na hivyo huenda Makgalwa akarejeaa tena benchi akisubiri nafasi yake.