Kocha Mkuu wa Simba, Steve Barker, ameweka wazi mpango wake wa kuhakikisha Mighty Wanderers wanapata wakati mgumu katika mchezo wa marudiano wa hatua ya awali ya Ligi ya Mabingwa Afrika (CAFCL), utakaopigwa kesho Jumapili, Septemba 13, 2026 katika Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.
Simba itaingia kwenye mchezo huo ikiwa na faida ya bao 1-0 iliyopata katika mchezo wa mkondo wa kwanza uliochezwa nchini Malawi, huku Barker akisisitiza kuwa kikosi chake kimejiandaa kufanya vizuri zaidi kuliko kilivyofanya ugenini.
Kocha huyo amesema maandalizi ya timu yanaendelea vizuri huku baadhi ya wachezaji waliokuwa na majeraha madogo wakirejea katika kikosi, jambo ambalo limeongeza chaguo kwa benchi la ufundi.
“Timu ipo kwenye hali nzuri, wachezaji wachache waliokuwa na majeraha madogo na matatizo wanarudi, hivyo tupo katika hali nzuri ya maandalizi ya mechi hii,” amesema Barker.
Barker amesema Simba inapaswa kuongeza kiwango katika mchezo huo wa marudiano, akitambua kuwa ushindi wa ugenini katika mashindano ya Afrika si jambo rahisi.
“Tunapaswa kuwa na kiwango bora zaidi kuliko tulichokuwa nacho ugenini Jumapili, lakini haikuwa mazingira rahisi. Ushindi wowote wa ugenini katika mashindano ya bara unapaswa kuonekana kama matokeo mazuri,” amesema.
Barker ataka dimba la Uhuru kuwa gumu kwa Wanderers
Barker anataka Uwanja wa Uhuru uwe sehemu ya presha kwa wageni, huku akiwataka wachezaji wake kuanza mchezo kwa kasi, kucheza kwa mtazamo wa kushambulia na kuwafanya wapinzani kushindwa kupata nafasi ya kucheza kwa utulivu.
Kocha huyo anaamini mazingira ya nyumbani pamoja na nguvu ya mashabiki yanaweza kuwa sehemu muhimu katika kuisukuma Simba kuelekea raundi ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa Afrika.
“Si rahisi kwa timu kuja Tanzania kucheza dhidi yetu. Tunahitaji kuhakikisha ni mazingira magumu kwao, ni vigumu kucheza dhidi yetu,” alisema Barker.
Simba inahitaji kulinda faida yake ya bao moja huku ikisaka ushindi mwingine mbele ya mashabiki wake ili kuhakikisha inakata tiketi ya kufuzu hatua inayofuata ya michuano hiyo mikubwa ya klabu barani Afrika.
Mchezo huo unatarajiwa kuwa na ushindani mkubwa kutokana na Mighty Wanderers kuhitaji matokeo ya kuwapa nafasi ya kugeuza hali ya mchezo baada ya kupoteza 1-0 katika uwanja wao nchini Malawi.