Kocha Mkuu wa Simba SC, Steve Barker, amesema ushindi wa bao 1-0 walioupata dhidi ya Mighty Wanderers ya Malawi katika mchezo wa kwanza wa hatua ya awali ya Ligi ya Mabingwa Afrika (CAFCL) haujawafanya kujiona tayari wameshamaliza kazi.
Barker amesisitiza kuwa wanahitaji kuonyesha kiwango bora zaidi katika mchezo wa marudiano.
Simba iliibuka na ushindi ugenini katika mchezo wa kwanza uliochezwa nchini Malawi, matokeo ambayo yameiweka katika nafasi nzuri kuelekea mchezo wa pili utakaopigwa kesho Jumapili, Septemba 13, kwenye Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam.
Akizungumza kwenye mkutano na wanahabari kuelekea mchezo huo, Barker amesema ushindi wa ugenini ni matokeo muhimu, lakini kikosi chake hakitakiwi kubweteka kwa faida hiyo, badala yake kinapaswa kuongeza kiwango mbele ya mashabiki wake.
“Tunahitaji kuonyesha kiwango zaidi mbele ya mashabiki wetu. Malengo ni kushinda na kwenda hatua inayofuata, ambayo itatupa nafasi ya kupigania hatua ya makundi msimu huu,” amesema Barker.
Barker amesema dhamira ya Simba ni kuhakikisha inapata matokeo yatakayoipa nafasi ya kusonga mbele katika mashindano hayo, huku ikilenga kufika hatua ya makundi msimu huu.
Libasse Gueye Arejea
Wakati huo huo, Barker amesema kurejea kwa mshambuliaji Libasse Gueye, ambaye alikosekana katika mchezo wa kwanza dhidi ya Mighty Wanderers, kumeongeza morali ndani ya kikosi.
Kocha huyo ameeleza kuwa uwepo wa Gueye ni nyongeza muhimu kwa timu kutokana na umuhimu wake katika mipango ya kiufundi ya Simba.
Simba itashuka dimba la Uhuru hapo kesho ikisaka matokeo yatakayoiwezesha kutinga raundi inayofuata ya CAFCL na kuendelea na safari ya kuwania nafasi ya kucheza hatua ya makundi.