Jana mshambuliaji wa Simba Ibrahim Doumbia alikuwa sehemu ya kikosi cha Wekundu hao wa Msimbazi walioibuka na ushindi mnono wa mabao 6-1 dhidi ya Mighty Wonderers katika mchezo wa mkondo wa pili hatua ya awali ligi ya mabingwa barani Afrika (CAFCL).
Simba iligawa dozi nene ikiondoka na ushindi wa jumla wa mabao 7-1 kufuatia ushindi wa bao 1-0 kwenye mchezo wa mkondo wa kwanza.
Bado Wanamsimbazi wanasubiri kushangilia bao la kwanza la Doumbia kwenye mechi za mashindano kwani kwa mara nyingine hakufanikiwa kuweka mpira kambani licha ya kutengenezewa nafasi kadhaa.
Jambo la uhakika ni kuwa, ni suala la muda tu Wanasimba watashangilia bao la mshambuliaji huyo kutoka Mali.
Katika mchezo huo pia kocha Steve Barker alimpa nafasi mshambuliaji Ismail Mgunda aliyesajiliwa kuchukua nafasi ya Suleiman Mwalimu aliyetimkia Yanga siku moja kabla ya dirisha la usajili kufungwa.
Mgunda alionyesha kiwango kizuri kwa muda mchache aliocheza akiongeza imani kwa Wanamsimbazi kuwa anaiweza kuifanya vyema kazi ya kuongoza safu ya ushambuliaji.

Mashabiki wa Simba wameendelea kuwaunga mkono washambuliaji hao ili kuhakikisha hawaondolewi mchezoni na presha za nje ya uwanja.
Doumbia kwa sasa anaonekana kufurahia zaidi sapoti anayopewa na mashabiki wa Simba, jambo linalomuongezea kujiamini.