Ligi Kuu ya NBC kesho inatarajia kushuhudia miamba miwili ya soka jijini Dar es salaam, Azam FC na Simba SC, itakapovaana katika dabi ya kukata na shoka maarufu kama 'Mzizima Derby', itakayopigwa kwenye Uwanja wa Azam Complex, Chamazi.
Mchezo huo unakuja huku Simba ikiwa na hesabu kali za pointi tatu ili kuendelea kujiweka katika nafasi nzuri kwenye msimamo wa ligi. Lakini mchezo baina ya timu hizo haujawahi kuwa mwepesi kwani timu zote mbili zimekuwa zikipishana vikali.
Rekodi zinasemaje?
Takwimu kutoka mechi 10 zilizopita za Ligi Kuu baina ya timu hizi zinaonesha kuwa hakuna mbabe wa wazi, jambo linalofanya mchezo wa kesho kutabirika kwa ugumu mkubwa.
Katika mapambano 10 yaliyopita, Simba SC imefanikiwa kuondoka na ushindi mara tatu (3), huku matajiri wa Chamazi, Azam FC, wakishinda mara mbili (2). Miamba hii imetoka sare katika michezo mitano (5).
Mechi ya mwisho kukutana ilikuwa Aprili 5, 2026, ambapo timu hizo zilitoshana nguvu kwa sare ya 0-0 kwenye uwanja huo huo wa Chamazi.
Hata hivyo, Azam FC wataingia uwanjani wakikumbuka ushindi wao wa mabao 2-0 walioupata ugenini dhidi ya Simba mnamo Desemba 7, 2025.
Akizungumza kuelekea mchezo huo, Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Simba Ahmed Ali amesema safari hii Simba imejipanga kuhakikisha haipotezi alama dhidi ya Azam Fc.
"Azam Fc ni miongoni mwa timu ambazo zimekuwa zikituvurugia hesabu zetu kwenye mbio za ubingwa, safari hii tumejipanga hatutaki kudondosha alama dhidi yao," alisema Ahmed.
Simba itaingia kwenye mchezo huo ikiwa na takwimu bora zaidi msimu huu kwani Wekundu hao wa Msimbazi wameshinda mechi zote tano za ligi kuu na mechi mbili za ligi ya mabingwa huku Azam Fc wakiwa tayari wamedondosha alama nne kwenye ligi.