Mwenyekiti wa Kamati ya Waamuzi, Nassoro Amduni amethibitisha kufungiwa kwa baadhi ya waamuzi kutokana makosa mbalimbali ya kujirudia kwenye Ligi Kuu
Alisema baadhi ya waamuzi waliofungiwa adhabu zao zipo ukingoni kumalizika na punde watarejea katika majukumu yao baada ya kupewa tena mafunzo ikiwa njia mojawapo ya kuboresha utendaji kazi wao.
Kauli yake ameitoa baada ya kuonekana taarifa mitandaoni ikieleza waamuzi 20, kati yao waamuzi wa kati 13 kuondolewa kwenye orodha katika michezo ya ligi iliyobaki na hawatakuwepo pia msimu ujao
"Ni kweli waamuzi takribani 20 wamekutana na rungu kupitia kamati ya mamlaka husika kwa kipindi tofauti na hiyo imetokana na makosa ambayo yamepelekea kupata adhabu hiyo"
"Kuna wengine wamesimamishwa kuchezesha kwa kipindi fulani, lakini kuna wengine wameondolewa kwenye ratiba, hivyo ukisema wamefungiwa ni sawa japo wametofautiana adhabu, wengine miezi sita, wengine miezi mitatu," alisema Amduni.
Aliongeza wengine baada ya kuondolewa wamerejeshwa kwenye kamati ya waamuzi kwa ajili ya kuwarekebisha kwa kupewa mafunzo upya kisha watarejeshwa kwenye ligi lakini hakuna mwamuzi aliyefungiwa hadi msimu ujao.
"Kuna waamuzi wameondolewa hadi mwishoni wa msimu, wengine michezo mitatu na msimu ujao hayo ni mambo mengine. Mfano Arajiga (Ahmed) ambaye msimu uliopita alikuwa mwamuzi bora alishasimamishwa na anakaribia kumaliza adhabu yake hivyo akimaliza tutampika upya na kumrejesha tena na adhabu hizi zinazotolewa ni endelevu"
Licha ya kutotaja majina ya waamuzi na adhabu zao lakini taarifa zilizokuwa zikizagaa zinamtaja pia Emmanuel Mwandembwa, Hussen Athuman, Nassor Mwinchui, Florentino Zablon, Elly Sasii, Arajiga, Amina Kyando na Rafael Ikambi
Waamuzi wa kati ni Jackson Palangyo, Hence Mabena, Hilbert Marine, Ahmed Simba wakati wa pembeni ni Mary Mwakitalama, Rashid Zongo, Hamis Chang’walu, Jesse Erasmo, Kassim Mapanga, Fredinand Chacha na Soud Lila