Kocha Mkuu wa Yanga Nasreddine Nabi amemtaka kiungo Feisal Salum kufikiria hatma yake katika kusakata kabumbu kwa kufanya uamuzi sahihi
Feisal amekuwa nje ya uwanja tangu mwishoni mwa Disemba 2022 baada ya jaribio lake la kuvunja mkataba na Yanga kukwama
Pamoja na Mtendaji Mkuu wa Yanga Andre Mtine kumuandikia barua kumtaka aripoti Avic Town kuendelea na majukumu yake kwa mujibu wa mkataba, Feisal bado hajaonekana
Nabi alifanya mazungumzo na mchezaji huyo kupitia simu na kumshauri amalize mgogoro wake na Yanga ili aweze kurejea kwenye majukumu yake
"Mimi ni baba namchukulia Fei au mchezaji yeyote niliyenaye kama mwanangu wa kiume Hedi, ukiangalia Yanga maisha yanaendelea, lakini maisha ya Feisal yamesimama na kipaji chake kimesimama"
"Nilimpigia, lakini niliongea na wachezaji wenzake nikamwambia kitu kikubwa sasa sio pesa tu anatakiwa pia kufikiria kuhusu kipaji chake, mtu bora ambaye atakuwa anamshauri vizuri ni yule atakayemwambia atafute nafasi ya kumaliza utofauti wake na klabu arudi kazini"
"Nafahamu athari za mchezaji kukaa nje bila kucheza mechi za mashindano, athari za mamna hiyo anaweza asizijue kwa undani mtu mwingine ambaye hachezi mpira wala hajacheza mpira, hata kama Feisal anataka kuondoka Yanga hiki kinachoendelea hakiwezi kumsaidia kitamuangamiza," Nabi alinukuliwa na gazeti la Mwanaspoti
Hivi karibuni Rais wa Yanga Injinia Hersi Said alisisitiza kuwa Feisal ni mchezaji wao mpaka May 2024



