Kocha Mkuu wa TP Mazembe Mihayo Kazembe amesema mchezo wao wa kombe la Shirikisho dhidi ya Yanga ambao utapigwa uwanja wa Benjamin Mkapa siku ya Jumapili, Februari 19 utakuwa mgumu
TP Mazembe walitua nchini Alhamisi jioni tayari kwa mchezo huo ambapo jana Ijumaa walifanya mazoezi yao ya mwisho katika uwanja wa Benjamin Mkapa ambao utatumika siku ya Jumapili
Kazembe amesema wanafahamu Yanga ina wachezaji wazuri ambao miongoni mwao wametoka DR Congo
"Yanga ni timu nzuri na yenye wachezaji wazuri, katika kikosi cha Yanga kuna wachezji wengi tu wazuri na wenye uwezo mkubwa wa kucheza mpira na kufanya maamuzi. Tunafahamu wachezaji wao baadhi ni Wacongo"
"Mchezaji kama Aziz Ki na hata Fiston Mayele ni wachezaji ambao wana majina makubwa na wanafanya vizuri tunaamini mechi haitakuwa rahisi lakini tumekuja hapa kushindana, muhimu kutafuta alama muhimu ugenini" alisema Kazembe
Kuelekea mchezo huo, Yanga inanufaika kwa kuwa na idadi kubwa ya wachezaji kutoka DR Congo ambao wamewahi kucheza dhidi ya TP Mazembe wakiwa na klabu ya AS Vita
Wachezaji kama Yannick Bangala, Djuma Shaban, Jesus Moloko, Tuisila Kisinda, Fiston Mayele na Joyce Lomalisa wamewahi kuitumikia AS Vita kabla ya kusajiliwa na Yanga
TP Mazembe ndio vinara wa kundi D wakiwa na alama tatu baada ya ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Real Bamako



