Muda unazidi kuyoyoma, majira ya saa 1 usiku Simba itashuka uwanja wa Benjamin Mkapa kuikabili Raja Casablanca katika mchezo wa ligi ya mabingwa barani Afrika
Ni mchezo wa pili kundi C, mchezo ambao unaweza kutoa taswira ya matumaini ya Simba katika mkakati wa kusonga mbele hatua ya robo fainali
Ni moja kati ya mechi tatu ambazo Simba watacheza uwanja wa nyumbani katika michuano hiyo, lengo likiwa kukusanya alama tisa
Mashabiki wa Simba hawajawahi kuwa na hofu na timu yao pale inapocheza uwanja wa Benjamin Mkapa
Sawa, ziko mechi chache ambazo Simba haikushinda nyumbani lakini mechi nyingi katika michuano ya ligi ya mabingwa, Mnyama aliunguruma dimba la Mkapa
Mashabiki wa Simba wanakwenda dimba la Mkapa wakiwa na matumaini makubwa kuwa timu yao leo itaendeleza rekodi yake ya kutumia vyema uwanja wa nyumbani katika michuano ya ligi ya mabingwa
Ni mechi muhimu sana kwa Simba kushinda, ikumbukwe Wekundu hao wa Msimbazi walipoteza mchezo wao wa kwanza dhidi ya Horoya Ac uliopigwa Guinea
Kuelekea mchezo huo, Meneja wa Habari na Mawasiliano klabu ya Simba Ahmed Ally amesema kuwa pamoja na kuwa mpira una matokeo matatu lakini leo wanahitaji tokeo moja tu, ambalo ni ushindi kwa Simba
"Leo kuna mambo mawili lazima yatokee uwanja wa Benjamin Mkapa, Simba kuifunga Raja Casablanca au Raja Casablanca kufungwa na Simba!," ni kauli ya shabiki kindakindaki wa Simba aliyejitambulisha kwa jina moja Rashid alipokuwa akitamba wakati akielekea dimba la Mkapa