Baada ya kurejea kutoka Uganda, Simba ilirejea mazoezini jana, Alhamisi March 02 itashuka uwanja wa Uhuru kuikabili African Sports katika mchezo wa kombe la FA ambao utapigwa saa 10 jioni
Mechi itakayofuata baada ya African Sports ni dhidi ya Vipers Fc ikiwa ni mechi muhimu ya ligi ya mabingwa Simba ikihitaji kushinda mchezo huo ambao utapigwa March 07 kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa ili kuweka hai matumaini ya kutinga robo fainali
Kocha Mkuu wa Simba Robertinho Oliveira anakiandaa kikosi chake kikamilifu akiweka wazi kuwa anahitaji kufanya maboresho hasa kwenye safu ya ushambuliaji akiwa haridhishwi na idadi ya mabao wanayofunga
Tangu kuanza hatua ya makundi, katika mechi tatu ambazo Simba imecheza, limefungwa bao moja tu tena kutoka kwa mlinzi wa kati Hennock Inonga Baka
Bado eneo la ushambuliaji halijazalisha mabao licha ya nafasi nyingi kutengenezwa
Robertinho amesisitiza kuwa wanahitaji kuongeza ufanisi kwenye eneo la mwisho kwa kutumia vyema nafasi wanazotengeneza
"Pamoja na ushindi ugenini lakini bado tuna tatizo katika eneo la mwisho. Baadhi ya nafasi tunazotengeneza zinapotea hilo linamuumiza kila mtu kati yetu na tunaenda kulifanyia kazi licha ya kwamba tumeshajua wapi tunaanzia"
"Katika mashindano yote tuliyopo tunahitaji mabao, hususani haya ya CAF ndio tunahitaji kufunga zaidi kwani inaweza kufika sehemu mkalingana alama na mwenzako na kitakachoamua kikawa mabao lazima tufanye kazi juu ya hilo," alisema Robertinho



