Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ameiagiza Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo kuanza haraka ukarabati wa Uwanja wa Mkapa ili ukidhi mahitaji yaCAF baada ya kuufanyia ukaguzi hivi karibuni
Mh Majaliwa alitoa agizo hilo jana Jumatano, Machi 1, 2023 jijini Dar es Salaam alipotembelea kukagua hali ya uwanja huo baada CAF kutaka ufanyiwe marekebisho katika baadhi ya maeneo
"Ili mradi CAF wametupa onyo, ni onyo ambalo wametupa na muda wa kufanya marekebisho na muda huo waliotupa ni lazima tuanze jambo ndipo waridhie mambo mengine yaendelee, nimekuja kuwaambia msiruhusu uwanja huu ufungiwe na CAF na kuzipeleka timu zetu zikacheze ugenini"
Waziri Mkuu alisema kuwa kwa kuwa CAF wameleta orodha ya makampuni yenye uwezo wa kufanya ukarabati wa kiwango cha juu hivyo Wizara itangaze zabuni ikiwezekana hata kwa mfumo wa 'Single Source' ili kazi ya awali ianze kufanyika katika maeneo ya kubadilishia nguo, vyoo, milango na bechi la ufundi
Aidha Mh Majaliwa ameagiza kufanyike mapitio ya idadi ya mechi zitakazokuwa zinaruhusiwa kutumia uwanja huo kwa kupunguza idadi ya mechi zinazochezwa kwa lengo la kutunza uwanja huo ikiwemo sehemu ya kuchezea
"Wizara, TFF na Bodi ya ligi fanyeni mapitio ya mechi zinazopaswa kuchezwa uwanja wa Benjamin Mkapa, Tunao uwanja wa uhuru na hata Azam Complex muda mwingi havitumiki pelekeni michezo mingine huko, hapa chagueni mechi ambazo zinaingiza mashabiki wengi"
Naye, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Said Yakubu amesema maeneo waliyoelekezwa na CAF kuyafanyia maboresho ni eneo la kuchezea (Pitch), benchi ya ufundi, vyumba vya wachezaji na waamuzi, ukumbi wa mikutano ya waandishi wa habari.
Maboresho mengine ni kubadili eneo la waandishi wanapokaa wakati wa mechi, kubadili muonekano wa viti sehemu ya VIP, kutenga chumba maalumu kwa ajili ya marejeo ya picha (VAR Room), kubadili Taa uwanjani na kuboresha uwezo wa jenereta kwenye uwanja.