Yanga imetakata uwanja wa Benjamin Mkapa jioni hii wakiibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Real Bamako katika mchezo wa kombe la Shirikisho
Mabao ya Fiston Mayele na Jesus Moloko yaliihakikishia Yanga alama tatu muhimu ambazo zimewaweka katika nafasi nzuri ya kutinga robo fainali ya michuano hiyo
Bao la kwanza la Yanga lilifungwa na Mayele kwenye dakika ya 8 akimalizia shambulizi lililoanzishwa na Kennedy Musonda
Mayele angeweza kufunga hata mabao matatu kwenye kipindi cha kwanza kama angeongeza umakini
Wakati wa mapumziko kocha Nasreddine Nabi alifanya mabadiliko muhimu akiboresha eneo la kiungo akimuingiza Khalid Aucho nafasi ya Aziz Ki huku Jesus Moloko akiingia nafasi ya Tuisila Kisinda aliyeumia
Mabadiliko hayo yaliiongezea Yanga ubora na kutengeneza nafasi zaidi ikiwemo mkwaju wa penati baada ya Mayele kufanyiwa madhambi katika eneo la hatari
Yannick Bangala alikosa mkwaju huo lakini kwenye dakika ya 68 Moloko akafunga bao la pili baada ya kumnyang'anya mpira mlinzi wa Bamako
Ni ushindi ambao umeifanya Yanga ifikishe alama saba na kujiimarisha katika nafasi ya pili
Yanga inahitaji kushinda mchezo dhidi ya US Monastir ili kufuzu hatua ya robo fainali
Mapema TP Mazembe ilikubali kipigo cha bao 1-0 kutoka kwa US Monastir sasa ikisalia nafasi ya tatu ikiwa na alama tatu





