Wakati leo inashuka ugenini kuwakabili Mbeya City katika mechi ya Ligi Kuu Bara itakayochezwa kwenye Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya, Ruvu Shooting imetangaza hali ya hatari katika mechi zake sita zilizobaki
Msemaji wa Ruvu Shooting, Masau Bwire, alisema mechi hizo ni za ukombozi kwa timu yao inayoburuza mkia na ahadi ya kupata matokeo chanya wanaianza leo watakapowavaa Mbeya City.
"Kikosi kiko jijini Mbeya muda mrefu, kiko huko kwa shughuli maalum ya kuhakikisha hizi mechi tulizosalia nazo zinaleta ukombozi kwenye klabu yetu, kwa hiyo ni lazima tujidhatiti, tujiweke vizuri ili tukae eneo salama, tuliwahi kwa lengo la kusoma mazingira yasije yakawaathiri vijana watapokuwa uwanjani wakiitetea timu yao," alisema Bwire
Alisema wameandaa mpango maalum wa kiufundi wa kuhakikisha timu hiyo haishuki daraja kwa kuimarisha umoja kuanzia kwa wachezaji, benchi la ufundi na viongozi wa timu hiyo.
Ruvu Shooting yenye pointi 17 imecheza mechi 24 na kati ya hizo imeshinda michezo minne, sare tano na kupoteza michezo 15.



