Yanga yaja na Full House, Full Shangwe

Joel JJ By Joel JJ β€’ 13th March 2023


Yanga yaja na Full House, Full Shangwe

Afisa Habari wa Yanga Ali Kamwe amesema wanawasiliana na Matawi ya klabu ya Yanga mikoani kuandaa utaratibu wa kusafiri kuja jijini Dar es salaam kushuhudia mchezo wa kombe la Shirikisho dhidi ya US Monastir ambao utapigwa Jumapili March 19 katika uwanja wa Benjamin Mkapa

Akizungumza katika Mkutano na Wanahabari mapema leo, Kamwe amesema wanatarajia kuwa na Mashabiki wengi kutoka mikoani hivyo amewataka Mashabiki wa jijini Dar es salaam 'wasilale' ili kuhakikisha Jumapili uwanja wa Benjamin Mkapa unajaa

"Tunawasiliana na Matawi ya Yanga mikoani ili kuweka sawa taratibu za safari za mashabiki kutoka mikoani wanaokuja kushuhudia mchezo dhidi ya US Monastir. Tunawaomba na wale wa jijini Dar es salaam msilale, mechi hii ni kubwa tuhakikishe tunaujaza uwanja wa Mkapa kuwahamasisha wachezaji wetu waweze kushinda siku ya Jumapili," alisema Kamwe

"Monastir tuna deni nao, na lazima tulipane. Sijui Monastir ametufungaje kule kwao. Pamoja na kutaka kufuzu lakini lazima deni lilipwe. Tunakwenda na FullHouse Full Shangwe waje tumalizane nao kwa Mkapa," alisema Kamwe

Kamwe ametangaza viingilio vya mchezo huo ni VIP A Tsh 30,000/-, VIP B Tsh 20,000/-, VIP C Tsh 10,000/- na Mzunguuko Tsh 3,000/-

Tiketi tayari zimeanza kuuzwa kwenye mifumo ya ununuzi wa tiketi kwa njia ya simu na Makao Makuu ya klabu ya Yanga, Jangwani

Kamwe ametangaza kauli mbiu kuelekea mchezo huo ni FULL HOUSE, FULL SHANGWE WAJE TUMALIZANE...!

Yanga itafanya tukio kubwa la Hamasa siku ya Jumatano, Manzese jijini Dar es salaam ambapo Wananchi watapata nafasi ya kununua tiketi na kupata burudani kutoka kwa Wasanii mbalimbali

Siku ya Ijumaa Yanga itaendesha zoezi la kuchangia damu Hospitali ya Mloganzila nje kidogo ya jiji la Dar es salaam

Siku ya Jumamosi, utaratibu wa 'jogging' kwa Wanachama na Mashabiki wa Yanga utaendelea kama walivyofanya katika mechi zilizopita

Siku ya Jumapili ambapo mchezo dhidi ya Monastir utapigwa saa 1 usiku, kuanzia saa 9 mchana kutakuwa na parade la robo fainali ambapo Wananchi wataandamana kutoka Jangwani kuelekea uwanja wa Benjamin Mkapa


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.