Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan, amezipongeza Klabu za Simba na Yanga kwa kuchangamkia fursa aliyotoa kwa kuahidi Sh. miioni 5 kwa kila bao kitakalofungwa kwenye michuano ya kimataifa ambayo zinashiriki
Rais Samia pia amewataka wachezaji wa timu hizo kuendelea kufunga mabao kwani fursa inaendelea na pesa bado zipo.
Akizungumza jana kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam, wakati wa maadhimisho ya kilele cha miaka miwili ya Uongozi wa Serikali ya Awamu ya Sita, iliyoandaliwa na Umoja wa Wanawake wa CCM Tanzania (UWT), Rais Samia alisema ndani ya miaka miwili ya uongozi wa awamu hiyo, michezo imenyanyuka kwa kiasi kikubwa na hii inatokana na umuhimu ambao serikali imeutoa kwenye shughuli za vijana, michezo na wasanii, mila na tamaduni za Mtanzania.
Akizungumzia ushiriki wa Simba Ligi ya Mabingwa Afrika na Yanga kwenye michuano ya Kombe la Shirikisho, Rais Samia alizipongeza klabu hizo kwa kufanya vema na kuipatia sifa Tanzania.
Wakati timu hizo zikienda kucheza mechi za raundi ya tatu, Rais alitoa ahadi ya Sh. milioni tano kwa kila bao litakalofungwa na timu hizo kwenye mechi zao za kimataifa.
"Lakini nipende kuwapongeza wanangu wa Yanga na Simba, nawapongeza kwa kutumia vizuri fursa niliowapa ya goli moja milioni tano. Wameitumia vizuri sana, kwa hesabu nilizonazo, nadhani Yanga wameshalamba milioni 30 na Simba jana (juzi) walichukua Sh. milioni 35, na huko nyuma nadhani walikula milioni 10, kwa hiyo niwapongeze kwa kuitumia vema fursa hiyo. Na ni imani yangu ile kasi iliyopo miguuni ya milioni tano kwa goli itaendelea kuwapo huko mbele, milioni tano zitakapoondoka," alisema Rais.
Pia alisema pesa bado zipo hivyo waendelee kutupia na hii ni baada ya juzi usiku Simba kushinda mabao 7-0 dhidi ya Horoya AC ya Guinea kuuona utani wa mashabiki wa soka uliokuwa ukiendelea kwenye mitandao ya kijamii.
"Niwahakikishie wale waliokuwa wakitania jana. Niliona utani, eti nampigia Msigwa (Gerson) namwambia eti maliza mpira haraka, mimi pesa zimeisha, nataka niwahakikishie mama bado anazo, endeleeni kuweka mpira kwenye wavu, bado zipo, wekeni mpira wavuni, jengeni jina la nchi yetu," alisema na kuzua shangwe kubwa uwanjani hapo. Msigwa ni Msemaji Mkuu wa Serikali ambaye ndiye mara zote huonekana kutoa pesa hizo kwa niaba ya Rais pale timu hizo zinapotekeleza kile walichoahidiwa.
Yanga ilikuwa imepata Sh. milioni 30 kabla ya mechi ya jana dhidi ya Monastir ya Tunisia ambayo walishinda mabao 2-0 na hivyo kufikisha milioni 40, Simba ikiwa imelamba Sh. milioni 45, hivyo tayari jumla ya Sh. milioni 85 zimeshatolewa na Rais Samia kwa jumla ya mabao 17 yaliyofungwa na timu hizo.