Mikiki mikiki ya ligi kuu ya NBC inaendelea leo kwa mechi mbili kupigwa jijini Dar es salaam
Saa 10 jioni KMC itakuwa uwanja wa Uhuru kumenyana na Geita Gold katika mchezo ambao KMC wanahitaji ushindi ili kujiondoa katika janga la kushuka daraja
KMC wako kwenye eneo la Play-off nafasi ya 14 wakiwa na alama 26 lakini hali ni shwari kwa wapinzani wao Geita Gold ambao wanashika nafasi ya sita wakiwa na alama 34
Saa 1 usiku mabingwa watetezi Yanga watakuwa uwanja wa Azam Complex, Chamazi kukabiliana na Kagera Sugar
Yanga inawania ubingwa wa 29 katika historia lakini Kagera Sugar nao wanahitaji ushindi ili kujiweka katika nafasi nzuri kuepuka hatari ya kushuka daraja
Ushindi wa mabao 2-0 ambao Simba waliupata dhidi ya Ihefu Fc hapo jana ni wazi umewaongezea presha Wananchi kuelekea mchezo huo kwani sasa wanaongoza ligi kwa tofauti ya alama tano, mambo yanaweza kuwa magumu kama watakosa ushindi leo
Simba na Yanga zitachuana kwenye mchezo wa dabi Jumapili, April 16, kama Yanga itapoteza leo na pia kufungwa na Simba ni wazi mbio za ubingwa zitakuwa wazi
