Kocha Rivers United atuma salamu kwa Wananchi

Joel JJ By Joel JJ β€’ 11th April 2023


Kocha Rivers United atuma salamu kwa Wananchi

Baada ya droo ya robo fainali ya michuano ya kombe la Shirikisho barani Afrika ambapo wawakilishi wa Tanzania katika michuano hiyo wakipangwa kukipiga na Rivers United katika hatua ya robo fainali, Meneja wa Rivers United, Stanley Eguma ametamba kuwa timu yake inafikiria kucheza fainali ya michuano hiyo

Rivers United watakuwa wenyeji wa mchezo wa kwanza unaotarajiwa kupigwa Aprili 23, mwaka huu nchini Nigeria, marudiano Aprili 30, mwaka huu jijini Dar

Eguma ametamba kuwa malengo aliyonayo ni kuona wanacheza fainali ya michuano hiyo msimu huu, hivyo hawezi kuona ugumu wa kucheza na timu yoyote katika hatua waliyofika kwa sasa

"Sina sababu ya kufikiria juu ya mchezo wetu wa robo fainali dhidi ya Yanga kwa sababu ni timu ambayo tunaifahamu, tulikutana msimu uliopita na kuwatoa, kitu kikubwa ambacho nataka kuona nafika fainali msimu huu."

"Yanga siyo timu mbaya, Kama wapinzani lazima tuwape heshima, lakini sioni sababu yoyote ya wao kuharibu mipango yetu na tushindwe kufikia malengo," alisema Eguma

Wakati Eguma akitamba, Kocha Mkuu wa Yanga Nasreddine Nabi amesema wanatambua mchezo dhidi ya Rivers United utakuwa mgumu lakini wamejipanga kuhakikisha wanashinda na kusonga mbele hatua ya nusu fainali

Nabi aliyerejea nchini hivi karibuni akitokea Tunisia kushughulikia masuala ya kifamilia, alisema anatambua Rivers United imebadilika tofauti na ile waliyocheza nayo msimu uliopita na kuwaondosha katika michuano ya ligi ya mabingwa

"Nafahamu Rivers United wamebadilika, wapo wachezaji wapya kwenye kikosi chao tofauti na wale tuliocheza nao msimu uliopita, lakini hata sisi tumebadilika sana, tuna timu imara zaidi kulinganisha na msimu uliopita"

"Jambo muhimu kwetu ni kuhakikisha tunajipanga ili tupate matokeo mazuri ugenini na kuhakikisha tunashinda nyumbani katika mchezo wa marudiano," alisema Nabi


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.