Simba yaipania Yanga dabi ya Kariakoo

Joel JJ By Joel JJ β€’ 12th April 2023


Simba yaipania Yanga dabi ya Kariakoo

Meneja wa habari na Mawasiliano klabu ya Simba Ahmed Ally amesema wana kila sababu ya kupata ushindi siku ya Jumapili katika mchezo wa ligi kuu dhidi ya Yanga ambao utapigwa April 16 katika uwanja wa Benjamin Mkapa

Akizungumza katika Mkutano na Wanahabari mapema leo, Ahmed alisema Simba imeingia rasmi katika wiki ya watani wa jadi ikiwa na dhamira ya kupata ushindi siku ya Jumapili

"Kwetu huu ni mchezo mkubwa sana. Lazima wachezaji wetu wajue wana kazi kubwa ya kuwarudishia furaha mashabiki wetu kwenye mechi hii ya Kariakoo Derby. Tunapata ushindi kwenye mechi ngumu zaidi, tutashindwaje kwa Yanga," alihoji Ahmed

"Sisi ndio wenyeji wa mchezo huo, tuna jukumu la moja kwa moja kutangaza mchezo huo, tunajukumu ya kutangaza maandalizi ya mchezo na timu"

"Kikosi kilirejea Dar jana usiku na leo kinaingia kambini. Jioni kitaanza mazoezi maalumu kuelekea kwenye mchezo, hali ya wachezaji ipo vizuri na hatuna majeruhi. Wachezaji waliopata majeraha kwenye mchezo dhidi ya Ihefu tuliocheza Dar wote wapo vizuri"

"Mechi itakuwa Aprili 16, 2023 saa 11:00 jioni. Viingilio tayari vimetangazwa na TFF. Tiketi tayari zinapatikana vituoni na kupitia mitandao ya simu," alisema Ahmed

Akizungumzia utaratibu wa tiketi, Ahmed amesema kwa mara ya kwanza wametambulisha aina mpya ya tiketi ili kuwarahisishia mashabiki kukidhi mahitaji yao

"Kwa mara ya kwanza kwenye mechi ya Kariakoo Dabi tutakuwa na tiketi za Executive. Tiketi itakuwa Tsh. 40,000 kwa mtu mmoja. Tutawapa gate pass na vinywaji wakiwa uwanjani. Tiketi zinauzwa kwa taasisi, mashirika au tawi na tiketi zinaanzia 20"

"Vile vile kwa mara ya kwanza tutakuwa na tiketi za Platinum. Tiketi moja ni Tsh. 150,000. Unapata usafiri kutoka na kurudi hotelini mkisindikizwa na polisi, chakula na vinywaji muda wa mapumziko pia kutakuwa na zawadi maalumu," alisema Ahmed

Simba pia imetambulisha Mnyama Tiketi ambapo kwa mujibu wa Mkurugenzi Mtendaji wa Simba, Imani Kajula, amesema tiketi hizo ni maalum kwa mashabiki ambao wanapenda kwenda pamoja uwanjani

"Kuelekea mechi ya watani wa jadi, Simba inatangaza aina mpya ya tiketi ambayo ni Mnyama Ticket ambayo itawezesha marafiki ambao wanapenda kwenda pamoja uwanjani wanaweza kununua tiketi kama kundi"

"Hatupendi mashabiki wetu ambao wana kundi kupata shinda ya tiketi. Namba zitapatikana kwenye ofisi za Simba. Tunawaondolea changamoto ya kupanga foleni. Tunaamini siku ya Jumapili uwanja utajaa rangi nyekundu na nyeupe. Bei zinategemea na eneo," alisema Kajula


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.