Derby ya Kariakoo itakuwa ngumu - Jembe Ulaya

Joel JJ By Joel JJ β€’ 14th April 2023


Derby ya Kariakoo itakuwa ngumu - Jembe Ulaya

Nyota wa zamani wa Yanga, Bakari Malima 'Jembe Ulaya' amesema mechi ya watani wa jadi nchini, Simba na Yanga itakayochezwa Jumapili kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam itakuwa na 'mvuto mkubwa' kutokana na aina ya usajili uliofanywa na timu hizo

Simba itakuwa mwenyeji wa mechi hiyo ya marudiano ya Ligi Kuu Tanzania Bara na mshindi atakuwa amejisafishia njia ya ubingwa wa msimu huu.

Jembe Ulaya amesema anaamini mechi hiyo itakuwa na ushindani na si nyepesi kwa upande wowote.

Jembe Ulaya alisema kila timu itatakuwa kuwa makini katika muda wote kwa sababu lolote linaweza kutokea ndani ya dakika hizo 90.

"Mchezo wa Simba na Yanga wa Jumapili unatarajiwa kuwa na mvuto wa aina yake kutokana na aina ya vikosi vilivyo sasa, timu zote zimeimarika kwa kiasi kikubwa tofauti na zilivyokuwa miaka ya nyuma, zimesajili wachezaji ambao wana viwango vya kimataifa na wanaocheza soka la ushindani," alisema Jembe Ulaya.

Nyota huyo ambaye kwa sasa anaifundisha timu ya vijana ya Yanga, alisema kwa upande wa Simba imeimarika zaidi baada ya kuwasajili wachezaji wa kimataifa, Saidi Ntibazonkiza na Jean Baleke, ambao wameongeza nguvu kwenye safu ya ushambuliaji.

"Sina mashaka na kikosi cha Yanga baada ya kumwona, Stephano Aziz Ki amerudi kwenye kiwango chake cha kawaida, tunaomba mashabiki wajitokeze kwa wingi uwanjani kuangalia burudani itakayotolewa na wachezaji wetu siku hiyo," mkongwe huyo alisema.

Timu hizo zinakutana zote zikiwa zimetinga hatua ya robo fainali ya mashindano ya kimataifa yanayoandaliwa na Shirikisho la Soka Afrika (CAF).


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.