Vilabu vinavyoshiriki Ligi Kuu ya Uingereza vimekubaliana kutoweka mbele ya jezi za wachezaji nembo za michezo ya kubahatisha kuanzia msimu wa mwaka 2026/7 katika michezo ya ligi hiyo maarufu duniani
Kuna timu nane katika ligi hiyo zinazodhaminiwa na makampuni ya michezo ya kubahatisha. Taarifa iliyotolewa na bodi ya ligi hiyo imesema vilabu vya EPL kwa pamoja wamepitisha azimio la kutoweka mbele ya jezi nembo za michezo hiyo wakati wa mechi za ligi.
Hatua hiyo inaifanya ligi hiyo kuwa ya kwanza kuchukua hatua hiyo ili kupunguza matangazo yanayochochea michezo hiyo.
Maamuzi ya bodi ya ligi hiyo yamehusisha wadau mbalimbali katika kuchukua hatua hiyo vikiwemo vilabu vyenyewe na serikali.
Bodi hiyo kwa sasa inahusisha pia wadau ili kuja na sera mpya itakayotoa mwongozo wa udhamini unaotokana na michezo ya kubahatisha.
Bodi hiyo imesema wakati watu wazima wanasikia raha kucheza michezo ya kubahatisha, matangazo ya michezo hiyo kupitia vilabu yamekuwa na athari kwa watoto wadogo ukizingatia kuwa wachezaji wamekuwa ni mfano wa kuigwa na mashabiki wa watoto hao.