Mlinzi wa kati wa Mabingwa wa Soka Tanzania Bara Yanga SC, Dickson Job amesema ilikua lazima aendelee kubaki klabuni hapo, ndio maana akasaini mkataba mpya wa kuendelea kuhudumu kwenye klabu hiyo
Job alikuwa anahusishwa na kujiunga na Vilabu vya Simba na Azam mwishoni mwa msimu huu, huku ikitajwa pia kuwa na dili zingine nje ya nchi, lakini Uongozi wa Young Africans mwishoni mwa juma lililopita ulimsainisha mkataba wa miaka miwili.
Dickson amesema ilikuwa lazima kwake kubaki Young Africans kwani ni timu ambayo amekuwa nayo kwenye wakati mzuri, pia imempa kile ambacho amekihitaji.
"Kikubwa ni kuwashukuru viongozi na mashabiki wote wa Young Africans kwa kuniamini na kuamua kuniongezea mkataba, nami kama mchezaji na nitaendelea kuipambania nembo kila ninapopata nafasi," amesema Job
Tangu aliposajiliwa Yanga SC, Beki huyo wa kati amekuwa katika kiwango kizuri ndani ya miaka miwili huku akiwa sehemu ya wachezaji wa kikosi cha kwanza na huku akibadilishana nafasi na nyota wengine wa nafasi hiyo kikosini akiwamo nahodha Bakari Mwamnyeto, Yannick Bangala na Ibrahim Abdullah 'Bacca'
Job mwenye bao moja katika Ligi Kuu Bara alikuwa kwenye sehemu ya wachezaji wa timu ya taifa ambayo inacheza michuano ya Kombe la Mataifa kwa Wachezaji wa Ndani (CHAN) na kwenye michezo ya kuwania kufuzu Fainali za Mataifa ya Afrika 'AFCON 2023'