Baada ya kukishuhudia kikosi chake kikichezea Bakora 2-0 mbele ya Mabingwa watetezi Tanzania Bara Young Africans, Kocha Mkuu wa Singida Big Stars Hans van der Pluijm, amesema hatakubali tena kufungwa na wababe hao wa Jangwani
Singida Big Stars Jumatano (Mei 04) ilishindwa kufurukuta katika Uwanja wake wa Nyumbani CCM Liti kwa kukubali kupigwa kichapo hicho ndani ya dakika 20 za kipindi cha kwanza, na kupelekea kuzitema alama tatu muhimu
Pluijm amesema kwenye mchezo ujao wa Kombe la Shirikisho la Azam 'ASFC' hatakubali kikosi chake kupoteza tena mbele ya Young Africans, kwa sababu atahakikisha anajipanga vizuri ili kushinda mchezo huo na kutinga Fainali ya michuano hiyo.
Amesema hata ikitokea anatinga Fainali ya michuano hiyo, pia hatakuwa tayari kupoteza mbele ya Simba SC au Azam FC ambapo moja kati ya timu hizo itaingia Fainali baada ya mchezo wa Nusu Fainali ya ASFC utakaochezwa leo Jumapili (Mei 07) mjini Mtwara
"Tulijipanga kushinda mechi zote mbili dhidi ya Young Africans, ila kwa kuwa tumefungwa huu hatutakubali kufungwa kwenye mchezo ujao tena, maana hamu yetu ni kuhakikisha tunacheza na fainali iwe na Simba au Azam atakae ingia," amesema Plujm
Young Africans na Singida BS zitachuana May 21 katika mchezo wa nusu fainali kombe la Shirikisho la Azam (ASFC) mchezo ambao uliahirishwa na TFF ili kuipa Yanga nafasi ya kujiandaa na mchezo Shirikisho CAF dhidi ya Malumo Gallants



