Meneja wa Habari na Mawasiliano klabu ya Simba Ahmed Ally amesema baada ya msimu huu kukamilika, mchakato wa maboresho ya kikosi kuelekea msimu ujao utaanza mara moja
Baada ya mabadiliko yaliyofanywa na Bodi ya Ligi, mechi za kuhitimisha msimu zitapigwa Juni 09 ambapo katika mwezi huo dirisha la usajili linatarajiwa kufunguliwa
Ahmed amesema uongozi wa Simba unafahamu kiu ya mashabiki ni kuona timu yao inaboreshwa zaidi ili kuhakikisha kilichotokea msimu huu hakijirudii msimu ujao
Aidha Simba itashiriki mashindano mapya ya Super League yatakayohusisha timu nane vigogo barani Afrika, hivyo kuwa na ulazima wa kufanya maboresho haraka ili benchi la ufundi lipate muda wa kutosha kukiandaa kikosi
"Uongozi unafahamu kiu ya mashabiki wa Simba ni usajili hasa kutokana na kile kilichotokea msimu huu ambao hatujaweza kushinda taji lolote"
"Uongozi unafanya kazi kwa karibu na benchi la ufundi ili kuhakikisha usajili utakaofanyika utazingatia mahitaji ya timu. Tunawaambia Wanasimba, tumejipanga safari hii tutaleta watu kwelikweli," alisema Ahmed
Tayari Simba imeanza kuhusishwa na baadhi ya wachezaji pamoja na kuwa kwa wakati huu bado ni tetesi tu