Azam Fc kwa sasa hawaifikirii fainali ya kombe la Shirikisho (FA) badala yake akili zao zipo kwenye michezo yao miwili ya mwisho ya ligi kuu Tanzania Bara ambapo wanataka kumaliza vizuri mechi hizo za mwisho msimu huu
Azam FC imetinga Fainali ya FA ikitarajia kucheza na Yanga kwenye Uwanja wa Mkwakwani mkoani Tanga, na kwenye ligi inashika nafasi ya tatu ikiwa na pointi 53 ikipishana kwa pointi mbili dhidi ya Singida Big Stars yenye pointi 51 wakivutana kumaliza katika nafasi hiyo.
Afisa Habari wa Azam FC, Thabiti Zakaria amesema kuwa wanachokiangalia hivi sasa ni mechi zao mbili za ligi kuhakikisha wanaibuka na pointi sita zilizobakia kwa kuwa fainali ya FA bado haijapangwa.
"Hii mechi ya FA bado hatujui itachezwa lini kwa sababu TFF bado hawajaipangia ratiba, hatuwezi kuifikiria kwa sasa, sisi tunaelekeza nguvu kwenye michezo yetu miwili ya mwisho kwenye ligi na baada ya hapo ndipo tutaanza mikakati kwa mchezo huo wa fainali baada ya kufahamu tarehe ya mchezo," alisema Zaka
Alisema kujiandaa na michezo hiyo miwili ya mwisho, awali waliweka kambi lakini baada ya bodi ya ligi kupangua ratiba waliamua kuvunja kambi na kuwapa wachezaji wao mapumziko mafupi.
"Lakini kwa sasa wachezaji wamerejea kwenye mazoezi kujiandaa na michezo hii miwili, malengo yetu ni kuhakikisha tunamaliza vizuri ligi msimu huu kwa kusanya pointi zote sita zilizosalia," alisema Zaka.
Bodi ya ligi imetangaza michezo ya mwisho kuhitimisha msimu huu wa ligi kuu itachezwa Juni 9.