Rais Samia abariki Tanzania kuandaa Afcon 2027

Joel JJ By Joel JJ β€’ 25th May 2023


Rais Samia abariki Tanzania kuandaa Afcon 2027

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kushirikiana na Kenya na Uganda kupitia Pamoja Bid wamedhamiria kuwa mwenyeji wa Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika zitakazofanyika mwaka 2027 (AFCON 2027), imefahamika rasmi

Akizungumza jijini, Dodoma jana, Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Zuhura Yunus, alisema nchi hizo zinawania nafasi hiyo kwa kutambua mafanikio makubwa ambayo sekta ya michezo imepata, hivyo kuwa wenyeji wa AFCON kutaongeza hamasa zaidi kwa ukuaji wa michezo hususan soka.

Alisema aidha michuano hiyo itachangia katika ukuaji wa utalii kwa kuwa ni mashindano ambayo hutazamwa na zaidi ya watu bilioni moja barani Afrika na maeneo mengine duniani kwa ujumla.

Vile vile, Rais Samia amesema mashindano hayo yataleta watu mashuhuri nchini wenye ushawishi duniani hivyo huwezesha na kunufaisha sekta nyingi za uchumi ambapo huchangia ajira, mapato kwa wafanyabiashara na serikali.

Kwa upande mwingine Rais Samia amesema Serikali kupitia Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kushirikiana na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), imeshafanya utafiti na kuandaa mpango mkakati wa utekelezaji wa maandalizi ya kuwa mwenyeji wa mashindano hayo.

Mashindano ya AFCON yataweka rekodi kwa mara ya kwanza kufanyika katika Ukanda wa Afrika Mashariki tangu yalipoanzishwa rasmi mwaka 1957.

Mwaka 2017, Tanzania ilikuwa mwenyeji wa Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika kwa vijana wa umri chini ya miaka 17 (AFCON U-17).


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.