Rasmi Sandaland The Only One amesaini mkataba wa miaka miwili kutengeneza na kusambaza jezi za klabu ya Simba
Thamani ya mkataba huo ni Tsh Bilioni 2 kwa mwaka, ikiwa ni mara mbili ya pesa ambayo Vunjabei aliweka
Akizungumza katika hafla ya kumtangaza Sandaland leo, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi Salim Abdallah 'Try Again' amemshukuru Vunja Bei kwa udhamini wake katika miaka miwili na kumkaribisha Sandaland
"Nampongeza Sandaland kwa kupata nafasi hii, alijaribu mara ya kwanza hakufanikiwa lakini muda huu amepata. Namshukuru pia VunjaBei kwa udhamini aliotupatia," alisema Try Again
Nae Mtendaji Mkuu wa Simba Imani Kajula amesema uongozi umefanyia kazi maoni ya Wanasimba kuhusiana na changamoto iliyojitokeza hapo awali na wana imani Mdhamini mpya Sandaland atamaliza changamoto hiyo

"Hatuwezi kuwa timu kubwa Afrika bila kuwa na uwezo wa kifedha, leo hii tunasimamia sana kwenye eneo hilo. Kwetu hatua ni safari na leo tunapiga hatua kubwa zaidi."
"Mashabiki walitwambia wanataka tuwe na jezi bora, zifike kwa wakati na zipatikane kila sehemu. Mwanzoni tulikuwa tunapata milioni 400 kwa mwaka kutokana na jezi. Akaja Vunja Bei akatupa bilioni moja kwa mwaka na huyu wa sasa anakuja kutupa bilioni mbili kwa mwaka. Namshukuru sana Sandaland kuwa mdhamini wa jezi kwa msimu wa 2023/24," alisema Kajula



