Mshambuliaji wa Yanga, Fiston Mayele ameeleza kushangazwa na watu wanaotaka aondoke kwenda timu nyingine wakati akiwa bado ana mkataba na klabu hiyo
Mayele ametoa kauli hiyo baada ya kuzisikia kauli za baadhi ya mashabiki hasa wa upande wa pili na wachambuzi ambao kila kukicha wanaibua tetesi za yeye kuondoka Yanga huku wengine wakimshauri aondoke
"Wakati nakuja hapa Tanzania hakuna mtu aliyenijua, nilichokifanya ni kujituma na nidhamu. Ninaipenda kazi yangu ndio maana leo kila mtu anamuimba Mayele"
"Nilisema tangu nikiwa mdogo malengo yangu ni kucheza mpira na nitafanikiwa kupitia soka, kwa sasa naona nimeanza kutimiza malengo yangu na kupata japo mafanikio lakini sijafikia hata nusu ya malengo yangu, nitaendelea kupambana zaidi"
"Ninawashangaa wanaotaka niondoke Yanga, watu wanasubiri kwa hamu 'Thank You' ya Mayele, mimi bado nina mkataba wa mwaka mmoja na Yanga na ninaheshimu mkataba wangu, ikija ofa tutakaa mezani tutazungumza,” amesema Mayele
Rais wa Yanga Injinia Hersi Said amesema jukumu la uongozi wake ni kuhakikisha wanawabakisha wachezaji wote muhimu kikosini
Tayari Yanga wamempa Mayele ofa ya mkataba mpya kukiwa na maboresho ya mshahara wake
Hata hivyo Yanga imeweka wazi msimamo wake kuwa iko tayari kuzingatia maamuzi yenye maslahi kwa pande zote mbili ikitokea kuna timu imewasilisha ofa nono zaidi