Mara baada ya wachezaji wa timu ya Al Hilal kutaka kusitisha mkataba huku wakihusishwa na baadhi ya timu, mabosi wao wameamua kuwafungulia mashtaka Fifa
Wachezaji waliositisha mikataba yao ni Fabrice Ngoma anayehusishwa Simba, Lamin Jarjou na Ibrahim Imoro ambao haijajulika wanajiunga na timu gani
Ngoma na wenzake wanadaiwa kusitisha mikataba yao kinyume na taratibu na hivyo Al Hilal kutangaza rasmi kuwafungulia mashtaka FIFA
Ngoma alijiunga na Al Hilal akisaini mkataba wa miaka mitatu ambao ameshautumikia kwa msimu mmoja
Hata hivyo hakuwa na wakati mzuri na matajiri hao wa Sudan kutokana na majeraha yaliyokuwa yakimsumbua mara kwa mara
Machafuko yaliyotokea huko Sudan imekuwa sababu kwake na wenzake kuvunja mikataba yao ingawa Al Hilal imedai kuchukua hatua kwa kuhamisha kambi ya timu hiyo nchini Misri ili kulinda usalama wa wachezaji
Al Hilal wako Tunisia wakishiriki michuano maalum ya nchi za kiarabu, nyota hao watatu hawakurejea kambini kuungana na wenzao
Imeelezwa Ngoma yuko jijini Dar es salaam kukamilisha usajili wake na Simba na alikuwa akisubiri barua kutoka Al Hilal ili mchakato huo ukamilike
Lakini kwa taarifa hiyo iliyotolewa na Al Hilal ni wazi timu hiyo haitawapa wachezaji hao barua mpaka mgogoro wao utakapotatuliwa na FIFA