Uongozi wa Singida Fountain Gate iliyopo Ligi Kuu Bara na itakayoshiriki michuano ya kimataifa ya Kombe la Shirikisho Afrika, umemuongezea mkataba wa mwaka mmoja kocha mkuu wa timu hiyo Mholanzi Hans Pluijm
Pluijm aliyeiwezesha timu hiyo kumaliza nafasi ya nne na kufuzu michuano ya CAF msimu ujao, alimaliza mkataba na klabu hiyo tangu Juni 30, mwaka huu jambo lililozua hofu juu ya hatima yake ndani ya kikosi hicho
Pluijm amesema amejisikia furaha kupewa mkataba huo huku akiahidi mambo makubwa msimu ujao licha ya kukiri ushindani utakuwa ni mkubwa kutokana na mashindano mbalimbali ambayo timu hiyo itakuwa ikishiriki
"Msimu wa kwanza ulikuwa ni mzuri kwetu kwa sababu tuliweza kufikia malengo tuliyojiwekea lakini bado tuna kazi kubwa ya kufanya hivyo kitendo cha kuongezewa mkataba ni ishara tosha viongozi wangu wananiamini ingawa kwangu ni deni,"alisema
Kwa upande wa Ofisa Mtendaji Mkuu wa timu hiyo, Olebile Sikwane amesema;
"Pluijm alianza na timu hivyo hatukuhitaji kufanya maboresho kwenye idara hiyo, tuna matumaini makubwa kwake na kama ambavyo nilisema tangu nimeteuliwa kwenye nafasi hii malengo yetu ni kuleta ushindani kwenye mashindano ya ndani na nje"



