Kocha Mkuu wa Yanga Miguel Gamondi amesema wamekamilisha maandalizi tayari kwa michuano ya ligi ya mabingwa hatua ya awali, kesho wakitarajia kuchuana na Asas Fc ya Djibout
Gamondi amesema pamoja na kuwa hawawafahamu vyema wapinzani wao, wamejiandaa kikamilifu tayari kwa kukabiliana nao kwani anaamini ni timu nzuri
"Tumekamilisha maandalizi ya mchezo wa kwanza wa ligi ya mabingwa dhidi ya Asas Fc. Hatuwafahamu vyema wapinzani wetu lakini tumefanya maandalizi kikamilifu naamini tutakuwa na mchezo mzuri na matokeo mazuri pia"
Gamondi amesema baada ya michuano ya Ngao ya Jamii, wamepata muda wa kufanya maboresho maalum ya kiufundi hivyo mashabiki wa Yanga watarajie burudani na mchezo mzuri utakaoambatana na magoli
Akizungumza kwa niaba ya wachezaji wenzake, mlinzi wa kushoto Nickson Kibabage amesema wanakwenda kwenye mchezo huo wakiwa na dhamira ya kushinda
"Sisi hatudharau timu yoyote, tunajua tunakutana na timu ambayo ni bingwa huko kwao hivyo tunauchukulia mchezo huu kwa uzito kama mechi nyingine yoyote," alisema
Mchezo huo wa mkondo wa kwanza hatua ya awali michuano ya ligi ya mabingwa barani Afrika, utapigwa Jumapili August 20 saa 11 jioni katika uwanja wa Azam Complex, Asas Fc wakiwa wenyeji wa mchezo huo