Kufuatia Ligi Kuu kutarajiwa kusimama mwishoni mwa wiki kupisha kalenda ya mechi za Kimataifa, wachezaji wa Simba walipewa mapumziko kuanzia jana Jumatano na watarejea kambini Jumapili
Awali Simba iliendelea na ratiba wa maandalizi yake ikiwa na matarajio ya Bodi ya Ligi kuridhia ombi la mchezo dhidi ya Coastal Union kupigwa siku ya Ijumaa lakini mchezo huo utapangiwa tarehe mwezi ujao baada ya kalenda ya mechi za Kimataifa
Afisa Habari wa TPLB, Karim Boimanda amesema imekuwa ngumu kubadili ratiba kutokana na muingiliano wa mechi ya timu ya Taifa Stars inayotarajia kuchezwa kuanzia Septemba 4 hadi 12 mwaka huu ambapo Stars watacheza na Algeria
"Ni kweli waliandika barua ya kuomba mechi ichezwe Ijumaa lakini sababu ya mechi hiyo kutopangiwa tarehe ama kutochezwa hiyo Ijumaa waliyoomba Simba ni kutokana na ratiba ya Taifa Stars ambao wana mechi ya kufuzu"
"Kikawaida kocha wa timu ya taifa anatakiwa aingize timu kambini wiki kama mbili kabla ya mechi. Sasa wiki hizi zipo ndani ya ratiba ya Taifa Stars, kikanuni pia ni kwamba timu ikitoa wachezaji watatu kwenda timu ya taifa basi mechi zake zinasogezwa na Simba huenda wakatoa wachezaji hao"
"Hivyo hapa ratiba inatubeba wote ili tuwe salama, bodi na timu, maana kama tungeipangia tarehe hiyo mechi na ikatokea Simba imetoa wachezaji zaidi ya watatu wana uwezo wa kugomea mechi kuwa hawatacheza wachezaji wao wapo timu ya taifa,"
"Hivyo hadi muda huu ratiba ipo pale pale, Simba wasubiri hadi bodi itakapopanga tarehe ya mechi hiyo, ukiangalia pia Coastal wamewapa mapumziko wachezaji wao," Boimanda amenukuliwa na gazeti la Mwanaspoti



