Mama Mzazi wa Stephane Aziz Ki, kiungo mshambuliaji wa Yanga, amefichua kuwa aina ya uchezaji wa Wananchi ilikuwa sababu kubwa kwa mwanawe kuichagua Yanga licha ya kuwa na ofa kutoka kwa watani zao Simba
Katika mahojiano maalum na Yanga TV, Mama Aziz alifichua vile Rais wa Yanga Injinia Hersi Said alivyoweza kumshawishi nyota huyo mwenye kipaji cha aina yake kujiunga na Yanga
Injinia Hersi alisafiri mpaka Morocco kwenda kufanya mazungumzo na Aziz Ki na baada ya mazungumzo yao, mchakato wa usajili wake ukaanza hatua kwa hatua mpaka akajiunga na Yanga
"Baada ya kucheza kwa mafanikio makubwa kwa miaka miwili pale ASEC Mimosas, kuna vilabu vinne vilileta ofa ya kumtaka Aziz, moja kutoka Misri, moja kutoka Morocco na nyingine mbili kutoka Tanzania"
"Yeye alitamani akacheze Misri ili aonekane na baadae aende Qatar kwani ndiyo ilikuwa ndoto yake akijua atapata pesa. Alisema anacheza mpira sawa lakini mkononi hana kitu, anataka acheze mpira apate pesa"
"Injinia Hersi Said alisafiri mpaka Morocco kuonana na Aziz wakazungumza kuhusu uwezekano wa kumsajili lakini asingeweza kusaini mkataba. Alirudi tulishauriana tukashirikisha ma watu wengine wakashauri kule Uarabuni kuna ubaguzi mkubwa, hivyo tukawa tumepiga chini ofa ya Misri na Morocco ikabaki Simba na Yanga"
"Aziz alisema amecheza na Simba Sc alipokuja Tanzania akiwa na ASEC Mimosas lakini hakupenda aina ya uchezaji wao, hivyo akaanza kufuatilia Yanga akaona wanacheza vizuri akavutiwa na staili yao ya uchezaji na mbinu zao uwanjani, mwisho wa siku akachagua Yanga"
"Hakuchagua Yanga kwa sababu ya pesa, kwa sababu amgetaka pesa angeenda Misri au Morocco ambao walikuwa na ofa kubwa kuliko ya Yanga, alichagua Yanga ili kukuza kipaji chake na kuonekana zaidi," alisema
Pamoja na kutokuwa katika ubora wake, msimu wake wa kwanza na Yanga ulikuwa mzuri kwani alipachika mabao tisa akishika nafasi ya pili katika vinara wa upachikaji mabao katika kikosi cha Yanga nyuma ya Fiston Mayele aliyefunga mabao 17
Aziz Ki ameuanza vyema msimu huu mpaka sasa akiwa na mabao mawili kwenye ligi kuu, akifunga bao na assist moja kwenye mechi ya awali ligi ya mabingwa pia akifunga bao katika mechi za Ngao ya Jamii