Kocha Mkuu wa Simba Robertinho Oliveira amesema bado ana kazi ya kuimarisha safu ya ulinzi ili kuhakikisha wanasahihisha makosa yaliyojitokeza katika mechi zilizopita
Juzi katika mchezo wa kirafiki dhidi ya Cosmopolitan Simba iliibuka na ushindi wa mabao 5-1, Robertinho hakufurahishwa na safu yake ya ulinzi kuruhusu bao hilo lililopatikana kupitia mkwaju wa penati baada ya makosa ya safu ya ulinzi
Katika mchezo huo Simba iliwakosa walinzi wake wa kati wawili Hennock Inonga na Kennedy Juma ambao wanakabiliwa na majukumu ya timu za Taifa
Robertinho amesema wana muda mzuri wa kufanya kazi katika kiwanja cha mazoezi kabla ya kuelekea Zambia
"Bado tuna changamoto kwenye safu ya ulinzi,unaona jinsi gani tunafunga mabao lakini wapinzani wanaweza kufunga pia, hii ni kutokuwa makini, nimewaeleza mabeki nini cha kufanya"
"Nina imani kipindi hiki tutakitumia vyema kwa kuweka mambo sawa kabla ya kuelekea michuano ya kimataifa ambako hatupaswi kufanya makosa tukaadhibiwa," alisema Robertinho
Simba inatarajiwa kucheza mechi nyingine ya kirafiki kabla ya kuelekea Zambia kuikabili Power Dynamos kwenye mchezo wa mkondo wa kwanza kuwania tiketi ya kutinga makundi ligi ya mabingwa



