Achana na matokeo ya mechi za jana za Ligi ya Mabingwa Afrika wakati Simba na Yanga zilipocheza ugenini Zambia na Rwanda, hapa Dar es Salaam leo jioni, Singida Big Stars ina jambo lake kwenye Uwanja wa Azam Complex wakati itakapoikaribisha Future ya Misri katika Kombe la Shirikisho
Mchezo huo utakaopigwa saa 10:00 jioni unazikutanisha timu hizo, huku Singida ikitinga hatua hiyo kwa kuitoa JKU ya visiwani Zanzibar kwa jumla ya mabao 4-3, ilihali wageni wakianzia raundi ya pili ya michuano hiyo inayoendeshwa na Shirikisho la Soka Afrika (CAF).
Kocha mkuu wa Singida inayoshiriki michuano ya CAF kwa mara ya kwanza, Ernst Middendorp akizungumzia mchezo huo alisema lengo ni kupata matokeo mazuri nyumbani ili kupunguza presha mechi ya ugenini ambayo itakuwa ngumu zaidi kwao tofauti na ya mwanzo
"Kwa uzoefu wangu hii michezo ya Afrika kila timu inatengeneza mazingira ya kushinda nyumbani, sasa hii ni fursa kwetu ya kutumia vizuri uwanja wetu kisha kujiandaa na marudiano yatakayoamua hatima yetu," alisema Middendorp



