Kikosi cha Simba kinaendelea kujifua Mo Simba Arena tayari kwa mchezo muhimu wa kuwania tiketi ya kutinga hatua ya makundi ligi ya mabingwa barani Afrika dhidi ya Power Dynamos
Mchezo huo utaunguruma siku ya Jumapili, Oktoba 1 katika uwanja wa Azam Complex majira ya saa 10 jioni
Wapinzani wao Power Dynamos tayari wameondoka Zambia kuja nchini ambapo timu hiyo ilitarajiwa kuwasili saa 12
Vijana wa Kocha Robertinho Oliveira wanajiandaa kushinda mchezo huo wakifahamu matokeo hayo yatatosha kuwapeleka makundi
Sare ya mabao 2-2 katika mchezo wa mkondo wa kwanza uliopigwa Zambia, yameiweka Simba katika nafasi nzuri ya kufuzu kwani hata matokeo ya 0-0 au 1-1 yatatosha kuwavusha wekundu hao wa Msimbazi
Mkufunzi wa Simba Robertinho amesema maandalizi kuelekea mchezo huo yanaendelea vizuri, anaridhishwa na ari, morali ya wachezaji wake
"Tunafanya maandalizi muhimu, lengo letu ni kucheza vizuri na kupata ushindi mnono. Tutacheza nyumbani mbele ya mashabiki wetu, hii ni mechi muhimu sana kwetu"
"Nafurahi wachezaji wako tayari, ari na morali yao mazoezini ni kubwa, wanafahamu kwa ukubwa wa klabu ya Simba, wanapaswa kushinda na kukata tiketi ya kutinga makundi"
"Najua mchezo hautakuwa mwepesi kwa sababu Power Dynamos ni timu nzuri lakini niwaambie, Simba ni timu kubwa barani Afrika na tutaonyesha ukubwa wetu," alisema Robertinho



