Licha ya kufanikiwa kuivusha Simba hatua ya makundi ya michuano ya ligi ya mabingwa barani Afrika, Kocha Mkuu wa timu hiyo Robertinho Oliveira yuko katika presha kubwa
Baada ya mchezo dhidi ya Power Dynamos uliopigwa uwanja wa Azam Complex jana na Simba kulazimishwa sare ya bao 1-1 matokeo ambayo yalitosha kuwapeleka makundi kwa faida ya mabao mawili waliyofunga ugenini, Bodi ya Wakurugenzi ya Simba ilikutana kwa dharura kujadili kile kilichoelezwa kutoridhishwa na kiwango cha timu
Msimu huu mashabiki wa Simba wanatoa malalamiko karibu kila baada ya mechi kutoridhishwa na kiwango cha timu yao licha ya kuendelea kufanya vizuri
Hofu iliyopo ni kwamba hakuna uhakika kama wataweza kufikia malengo yao ya kucheza nusu fainali ya ligi ya mabingwa kama timu yao itaendelea kucheza ilivyo sasa
Miongoni mwa waliotoa malalamiko ni Rais wa heshima wa klabu ya Simba Bilionea Mohammed Dewji ambaye kupitia ukurasa wake wa mtandao wake wa kijamii aliandika ujumbe unaoashiria haridhwi kile alichokishuhudia
Katika misimu iliyopita, Simba ilidumisha utamaduni wake wa kucheza kandanda safi iliyoambatana na ushindi na zaidi kwenye michuano ya Kimataifa Simba imejijengea heshima ya kuwa timu hatari sana inapocheza mbele na mashabiki wake
Robertinho amekuja na falsafa tofauti ambapo jambo muhimu kwake ni timu kupata matokeo mazuri pasipo kujali wamecheza vipi
Mpaka sasa Robertinho amefanikiwa katika mbinu zake, hajapoteza mchezo katika mechi tisa zilizopita
Mwanzoni mwa msimu huu aliiongoza Simba kutwaa Ngao ya Jamii na ameweza kushinda mechi zote tatu katika ligi kuu
Hata hivyo presha ya mashabiki ambao wanataka 'bira biriyani' inaweza kupelekea akaondoshwa katika nafasi yake



