Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Mji Geita, Zahara Michuzi amemtaka Kocha Mkuu wa timu ya Geita Gold yenye maskani yake Mkoani Geita, Hemedi Suleiman, kufika ofisini kwake kwa lengo la kutolea ufafanuzi juu matokeo mabovu na sababu ya timu hiyo kutofanya vizuri
Kwa mujibu wa AyoTV, Zahara amesema haridhishwi na mwenendo wa timu hiyo huku akimtaka Kocha na benchi lake la ufundi wafike kumueleza vikwazo vinavyokwamisha timu hiyo kutofanya vizuri
"Nimetoa wito na angalizo kwa Mwalimu wa timu ya Geita Gold FC, kwanza anione kabla sijamtafuta, yeye pamoja na benchi lake la ufundi, kabla ya hatua yeyote tunaweza tukazungumza, kujua kwamba tunakwama wapi"
"Sisi kama Halmashauri Wamiliki wa ile timu hatujawajibika wapi, labda tunamkwamisha Mwalimu lakini niwahakikishieni timu ile sisi kama Halmashauri tumewajibika kadri ya uwezo wetu kuhakikisha inafanya vizuri," alisema
Zahara amekiri matokeo ya suluhu waliyoyapata Geita Gold FC ugenini Mkoani Mbeya dhidi ya Tanzania Prisons yanatoa mwanga wa mabadiliko lakini lazima hatua thabiti zichukuliwe kumaliza ukata wa matokeo mazuri
"Kama changamoto ipo kwa Wachezaji basi na kwenyewe tutachukua hatua, hakuna mkubwa zaidi ya Mwajiri na Mwajiri ni Halmashauri"
Ikumbukwe kuwa Geita Gold FC inafundishwa na Kocha Hemedi Suleiman Morocco ambaye tangu apewe dhamana hiyo, imecheza michezo nane ya ligi kuu ya Tanzania bara na kupoteza michezo minne, kupata sare tatu na ushindi mmoja pekee.



