Wachezaji Mudathir Yahya wa Yanga na Feisal Salum (Fei Toto) wa Azam wametozwa faini ya Sh2 milioni kila mmoja kwa kosa la kukataa kupeana mikono na waamuzi na wachezahu kabla ya mechi ya Yanga vs Azam kuanza Oktoba 22 Uwanja wa Mkapa
Katika taarifa ya Bodi ya Ligi imeeleza wachezaji hao walisimama katika mstari wa kuingia kiwanjani muda wa kupeana mikono kisha kuingia baada ya zoezi hilo kukamilika
Katika mechi hiyo mwamuzi namba moja, Janeth Balama wa Iringa amesimamishwa mizunguko mitatu kwa kosa la kushindwa kutafsiri sheria za mpira wa miguu
Aidha, mshambuliaji wa Singida Big Stars, Habib Kyombo ametozwa faini ya Sh1 milioni kwa kosa la kufanya vitendo vinavyoashiria imani za kishirikina katika mechi dhidi ya Namungo
Bodi ya Ligi pia imeelezwa kusikitishwa na kitendo cha ukatili na vurugu kilichofanywa na mashabiki waliokuwa wamevaa jezi ya Simba na bluu kumshambukia shabiki wa Yanga katika mechi ya Simba vs Ihefu Uwanja wa Mkapa
Bodi kwa kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama inakamilisha mchakato wa kuwatambua mashabiki wote waliohusika na tukio hilo kabla ya kuwachukulia hatua kali
Katika ligi ya Championship, Mchezaji Gilbert Boniface wa Cosmopolitan inayoshiriki Ligi ya Championship nchini Tanzania amefungiwa mechi 10 na faini Sh500,000 kwa kosa la kumshika mwamuzi sehemu za siri kwenye mechi dhidi ya Ken Gold wakati akipinga maamuzi ya mwamuzi huyo
"Baada ya tukio hilo mwamuzi alimuonyesha kadi nyekundu mchezaji huyo, ambaye alimfata na kumpiga teke kabla ya kutoka nje," imeeleza taarifa ya Bodi ya Ligi