Kocha Mkuu wa Yanga Miguel Gamondi amesema ana matumaini makubwa kikosi chake kitafanya vizuri kwenye mchezo wa ligi kuu dhidi ya Simba ambao utapigwa kesho Jumapili kaatika uwanja wa Benjamin Mkapa
Gamondi amesema amekuwa na wiki nzuri ya maandalizi, wachezaji wote wako tayari kwa mchezo huo
"Ninafurahi kuwa sehemu ya mchezo huu, tumejiandaa vizuri na tumekuwa na wiki nzima ya maandalizi. Nina imani na wachezaji wangu, kesho tutakuwa na mchezo mzuri, kila mshabiki wa soka atafurahia mchezo"
"Ni wazi mchezo wa kesho utakuwa tofauti na mchezo wa kwanza tuliocheza kwenye Ngao ya Jamii. Tunacheza katika uwanja mzuri na kila timu iko katika kiwango bora baada ya kucheza mechi kadhaa za ligi"
"Tunahitaji kushinda mchezo huu kwa sababu alama tatu zitatuhakikishia kuwa juu ya msimamo wa ligi. Najua ni derby lakini kwangu ni alama tatu muhimu," alisema Gamondi
Gamondi amesisitiza kikosi chake kina wachezaji bora na wenye uzoefu na ana matumaini makubwa watashinda mchezo huo
Akizungumza kwa niaba ya wachezaji wenzake, mlinzi wa kati Dickson Job amesema wamejiandaa vyema kuwania alama tatu katika mchezo huo
"Kwa upande wetu wachezaji tuko tayari kwa asilimia 100, walimu kwa upande wao wamemaliza kile walipanga kutuelekeza, imebaki kwetu wachezaji kutekeleza uwanjani," alisema Job



