Mdhamini na Mfadhili wa Klabu ya Yanga Ghalib Said Mohamed leo amefanya tukio la aina yake katika kumbukumbu ya siku ya kuzaliwa kwake
Hafla Maalum ya kusherehekea kumbukumbu ya kuzaliwa GSM imefanyika kwenye taasisi ya Kansa ya Ocean Road
GSM amechagua siku hii kusherehekea na wagonjwa wa kansa ambapo amechangia vifaa mbalimbali vya vipimo na matibabu ya magonjwa ya kansa
Akizungumza katika hafla hiyo, Rais wa Yanga Injinia Hersi Said alisema GSM ametoa msaada wenye thamani ya Tsh Milioni 137 kwa Taasisi hiyo
"Leo ni siku maalumu ya kuzaliwa kwa GSM. Siku hii angeweza kusheherekea kwa namna tofauti, lakini kwa mapenzi aliyo nayo kwa jamii ameona thamani ya kusheherekea na wenyewe uhitaji"
"Leo ameamua kutoa msaada wenye thamani ya Tsh Milioni 137. Wazo hili la kusaidia wahanga wa maradhi ya kansa, lilianza kwa Mke wake Salha"
"Mafanikio ya klabu ya Yanga kwa zaidi ya asilimia 80 yamechangiwa na uwepo na Ghalib Said Mohamed. Tunamshukuru sana GSM yeye pamoja na familia yake. Ametutoa mbali sana na tunaendelea kumsihi aendelee kuinga mkono klabu hii. Nasi tutamuombea katika kila hatua kwenye maisha yake," alisema Hersi
Hafla hiyo pia ilihudhuriwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mh Albert Chalamila ambaye amempongeza GSM kwa moyo wake wa kujitolea kwa watu wenye uhitaji
"Ndugu yangu ya GSM kwa hali ya maisha ulivyofikia sasa wala huhitaji mambo mengi tena, unahitaji mambo mawili tu, uwe karibu na Mungu na pili uwe na afya njema. Haya unayofanya leo, Mungu lazima atakupa mtaji wa afya, ili uweze kusaidia wengine zaidi. Usiache kutenda matendo haya ya huruma kwa jamii"
"GSM leo amechangia Tsh 137m kwa ajili ya kusaidia wahanga wa Kansa hapa Ocean Road. Hapa tunapata ujumbe mzito sana, wakati mwingine pesa hupotea lakini matendo huruma hudumu. Wote mliobarikiwa kuwa na uchumi mzuri tuzidi kutenda matendo ya huruma kwa jamii," alisema Chalamila



