Rais Samia aiagiza TFF igharamie kukarabati viwanja

Joel JJ By Joel JJ • 28th November 2023


Rais Samia aiagiza TFF igharamie kukarabati viwanja

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. Dkt. Samia Suluhu Hassan ameipongeza timu ya taifa ya vijana ya Zanzibar chini ya miaka 15 ‘Karume Boys’ kwa kutwaa ubingwa wa CECAFA U15 Boys Championship 2023

Akitoa pongezi hizo mwishoni mwa juma lililopita, Dkt. Samia pia alitoa neno kwa viongozi wa vyama vya michezo nchini kufanya uwekezaji kwenye soka la vijana 

“Michezo ni biashara kubwa, viongozi wa michezo badilikeni ili michezo iendeshwe kwa weledi. Tuache kutegemea kuvuna tusipopanda na kuweka mipango endelevu kwenye michezo ya vijana, mabaraza ya michezo yaendelee kuratibu na kufatilia utendaji wa vyama vya michezo na kuhakikisha vinaendeshwa na kujiendesha kwa manufaa ya taifa sio manufaa yetu binafsi," alisema Rais Samia

Aidha Rais Samia alitoa agizo kwa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kuhakikisha wanatenga fedha za ukarabati wa uwanja wa Benjamin Mkapa pale inapohitajika

"Ujenzi wa miundombinu ya viwanja vya kichezo ni gharama kubwa, viwanja vyote vinavyojengwa na kukarabatiwa vitumike kwa uangalifu na kufanyiwa marekebisho pale uharibifu unapojitokeza badala ya kusubiri hadi uharibifu mkubwa jambo ambalo linaongeza gharama mara dufu"

"Kuna kipindi nililetewa gharama za kukarabati uwanja wa Benjamin Mkapa, nikauliza kwani TFF wako wapi, wao si ndio wanatumia huo uwanja? Watu wanaoingia uwanjani wanalipa viingilio, hiyo pesa iko wapi?"

"Nikawaambia wawaambie TFF ule uwanja unajichumia pesa, hizo pesa kama walishazitumia wazitafute wakatabati uwanja. Kwa bahati kulikuwa na mashindano hapo mbele ikabidi tutoe fedha tukarabati uwanja"

"Lakini huo ndio msimamo wangu na ndio nitakao mwambia Rais Mwinyi asimame nao. Viwanja hivi vinaingiza pesa, sasa yale mafungu mnayojipangia muweke na fungu la viwanja ili vinapoharibika mnawahi kutengeneza," alisema Rais Samia


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.