Jioni ya leo Yanga itakuwa uwanja wa Baba Yara katika Mji wa Kumasi kuikabili Medeama Fc katika mchezo wa ligi ya mabingwa barani Afrika, raundi ya tatu kundi D
Hii ni mechi muhimu sana kwa Yanga kuzisaka alama zote tatu huko ugenini katika mchezo ambao unatarajiwa kuwa mgumu
Akizungumza katika Mkutano na Wanahabari jana, Mkufunzi wa Yanga Miguel Gamondi aliweka wazi kuwa kikosi chake leo kitashuka dimbani wakiwa na dhamira moja, kusaka ushindi
Yanga imedhamiria kutinga robo fainali ya michuano ya ligi ya mabingwa, ili kufanikisha hilo Wananchi wanahitaji kukusanya angalau alama 9 kutoka mechi nne zilizosalia
Kama Yanga itashinda leo, itafikisha alama nne huku ikiwa na mechi mbili nyumbani ambazo kama itashinda itafikia malengo ya alama 10
Hautakuwa mchezo rahisi kwa kuwa hata Medeama Fc wana hesabu zao za kushinda mechi zote nyumbani
Walishinda mchezo uliopita dhidi ya CR Belouizdad na leo watashuka tena uwanjani kusaka ushindi wa pili
Kwa hakika zitakuwa dakika 90 za kutoka jasho jingi kwa wachezaji wa Yanga ili kuhakikisha ushindi unapatikana na kama sio ushindi basi hata sare lakini sio kupoteza mchezo huo kwani wakipoteza watafifisha matumaini ya kusonga mbele katika michuano hiyo