Kocha Mkuu wa Simba, Abdelhak Benchikha, raia wa Algeria ambaye alitua na msaidizi wake Farid Zemiti na kocha wa viungo Kamal Boudjenane amempa mzawa, Seleman Matola jukumu la kupendekeza na kusajili wachezaji wazawa kwenye dirisha hili la Januari.
Matola ambaye ana mkataba wa kuifundisha timu ya vijana ya Simba, alirudishwa timu kubwa baada ya kuondolewa kwa kocha Robertinho Oliveira hivyo uongozi wa Simba ulimpa nafasi hiyo Matola na Daniel Cadena kukaimu hadi walipompata kocha mpya.
Habari za ndani katika uongozi wa Simba ni kuwa Benchikha ameridhia kumpa jukumu hilo Matola ambaye ni mchezaji wa zamani wa Simba, kwani anawajua vizuri wachezaji wa ndani zaidi yake na Bodi ya Wakurugenzi ya Simba pia imebariki suala hilo.
Matola atashirikiana na Cadena kuandaa ripoti nzima ya kikosi na kutoa mapendekezo ya nani abaki na nani waachane nao katika kipindi hiki cha usajili wa dirisha dogo unaofunguliwa rasmi Desemba 16, mwaka huu
Benchikha anaendelea kukifanyia tathmini kikosi chake lakini ni wazi katika dirisha dogo la usajili kuna nyota wapya wachache wataongezwa lakini usajili mkubwa zaidi utafanyika katika dirisha kubwa litakalofunguliwa Juni/Julai 2024



