Kikosi cha Simba kimerejea Tanzania usiku wa kuamkia leo wakitokea Ivory Coast walikofanikiwa kupata alama moja muhimu katika mchezo wa ligi ya mabingwa dhidi ya Asec Mimosas uliomalizika kwa matokeo ya suluhu ya bila kufungana
Akizungumza muda mfupi baada ya timu kutua JNIA, Kocha Msaidizi wa Simba, Suleiman Matola alisema akili na mahesabu yao wanayaelekeza kwenye mchezo wa Machi 2 dhidi ya Jwaneng Galaxy
Simba inahitaji kushinda mchezo huu ili iweze kutinga robo fainali ya tano katika miaka sita
"Tulihitaji kushinda mchezo dhidi ya Asec lakini naweza kusema tulikosa bahati lakini vijana walipambana nafikiri wote mliona" alisema Matola na kuongeza,
"Tunakwenda kufanya maandalizi kuelekea mchezo wetu wa mwisho ambao kwetu ni kama fainali, kuna mambo mawili katika mechi dhidi ya Jwaneng Galaxy kutafuta ushindi utakaotupeleka hatua ya robo fainali na kulipa kisasi"
"Hii haitakuwa mechi ya kawaida bali ni fainali kwetu kuhakikisha tunafikia malengo yetu ya kwenda robo fainali," alisema Matola.
Simba haitakuwa tayari kurudia makosa ya msimu wa 2020/2021 kwa kupoteza nyumbani dhidi ya Jwaneng Galaxy na kukosa nafasi ya kutinga hatua ya makundi ya ligi ya mabingwa na badala yake kuangukia katika kombe la Shirikisho ambako walifanikiwa kufika robo fainali
Simba itahitaji ushindi wa aina yoyote kutinga robo fainali pasipo kujali matokeo ya mchezo kati ya Wydad dhidi ya Asec



