Simba yatamba, Jwaneng lazima apigwe

Joel JJ By Joel JJ β€’ 28th February 2024


Simba yatamba, Jwaneng lazima apigwe

Meneja wa Habari na Mawasiliano klabu ya Simba Ahmed Ally amesema Simba itafuzu robo fainali ya michuano ya ligi ya mabingwa barani Afrika siku ya Jumamosi kwa kuibuka na ushindi dhidi ya Jwaneng Galaxy

Akizungumzamapema leo katika uzinduzi wa Hamasa Tawi la Tuna Wakera lililopo Keko Maduka Mawili, Ahmed alisema Simba haijawahi kufeli inapokuwa na jambo lake

"Jumamosi tunakwenda kuingia robo fainali kwa mara ya tano mfululizo, kwetu sisi kuingia robo ni jambo la kawaida. Tumezoea kucheza robo na hatujawahi kuishia makundi tangu tumeanza kampeni yetu ya kimataifa"

"Tulimuua AS Vita wa moto, tulimuua USGN, tulimuua Horoya hatuwezi kushindwa kwa Jwaneng Galaxy. Simba anapoitaka robo fainali hakuna wa kutuzuia hata timu zingine zote duniani zitengeneze timu moja"

"Jwaneng amekuja wakati mbaya, muda ambao tunataka kulipiza kisasi. Lilitukaa rohoni lakini muda wa kumtemea nyongo Jwaneng Galaxy, tulikaa na maumivu kwa miaka mitatu na la pili tunataka kuingia robo fainali"

"Hatuwezi kufungwa na timu inayoburuza mkia katika kundi letu. Tutafanya kila kinachowezekana ilimradi Simba ipate ushindi siku hiyo na hakuna kinachoshindikana. Iwe ardhini, angani au chini ya bahari"

"Tunawaahidi na kuwahakikishia Wanasimba kama kuna kitu kinahitajika hata kiwe kinapatikana chini ya bahari tutakifanya ili Simba iende robo fainali. Jumamosi ni kwenda kumalizia kazi"

"Robo fainali wamefuzu watu washambawashamba sembuse sisi. Hatuwezi kushindwa kwenda robo fainali, yani waporipori wamefuzu alafu sisi wenye mashindano tushindwe? Jumamosi saa 1 usiku tunakutana kumaliza kazi," alitamba Ahmed


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.