Kocha Mkuu wa Simba Abdelhak Benchikha amependekeza kikosi chake kuweka kambi ya muda mfupi visiwani Zanzibar kwa ajili ya maandalizi ya mchezo wa robo fainali ligi ya mabingwa dhidi ya Al Ahly ambao mkondo wa kwanza utapigwa uwanja wa Benjamin Mkapa, March 29
Meneja wa Habari na Mawasiliano klabu ya Simba Ahmed Ally amesema uongozi umepokea mapendekezo ya Benchikha na huenda wakaelekea Zanzibar kuweka kambi hiyo
"Ni kweli kocha wetu (Benchikha) amependekeza timu kuweka kambi ya maandalizi ya mchezo dhidi ya Al Ahly visiwani Zanzibar"
"Kocha amehitaji mazingira ya utulivu ili kuiandaa timu vyema kuhakikisha tunashinda mchezo huo. Uongozi umepokea mapendekezo hayo na tunaweza kuelekea Zanzibar," alisema Ahmed
Simba imepania kutinga nusu fainali ya ligi ya mabingwa na mkakati ni kuhakikisha ushindi mnono unapatikana katika mchezo wa kwanza utakaopigwa uwanja wa Benjamin Mkapa Ijumaa ya March 29



