Klabu ya Azam Fc imepania kulipa kisasi dhidi ya Namungo kutokana na kupoteza mechi ya nyumbani ya mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu Tanzania Bara
Oktoba 27, mwaka jana Azam ikiwa kwenye Uwanja wa Azam Complex, Dar es Salaam ilikubali kipigo cha mabao 3-1 dhidi ya Namungo
Mkuu wa Idara ya Mawasiliano wa Azam, Thabit Zacharia, alisema moja kati ya mechi muhimu zaidi msimu huu kwao katika Ligi Kuu Bara ni dhidi ya Namungo itakayochezwa Jumapili mkoani Lindi
Zaka alisema mbali na kuhitaji pointi tatu kutokana na vita kali iliyopo juu kati yao na vigogo, Simba na Yanga, lakini wanahitaji kulipiza kisasi kwa sababu hawaelewi sababu iliyofanya wakafungwa katika mechi wa kwanza
"Ni mchezo muhimu kwetu japo tupo juu ya Simba, lakini tuko huko kwa sababu tumecheza michezo mingi zaidi, hivyo hatutakiwi kupoteza michezo iliyobaki, hatutakiwi kuangusha pointi zaidi kwa sababu kuna wenzetu tumewazidi lakini wana michezo michache"
"Halafu kisasi ni haki, tunakwenda kulipiza kisasi kwa sababu mchezo wa kwanza walitufunga hapa kwetu Azam Complex," alisema Zaka Zakazi
Azam FC inakwenda kucheza mechi hiyo ikiwa nafasi ya pili kwenye msimamo, ikiwa na pointi 47, nyumba ya Yanga inayoongoza kwa pointi 52 na juu ya Simba iliyo nafasi ya tatu yenye pointi 45. Hata hivyo, Azam imecheza mechi mbili zaidi ukilinganisha na Simba, ikiwa imeshuka dimbani michezo 21, Wekundu wa Msimbazi wakicheza mechi 19 mpaka sasa.



