Klabu ya Yanga leo imeingia makubaliano ya ushirikiano na Bank ya NBC ambapo kupitia ushirikiano huo, Wanachama na Mashabiki wa Yanga wanaweza kujisajili na kulipa ada za uanachama katika benki ya NBC. Ni ushirikiano ambao Yanga pia imeingia na mabenki mengine kama CRDB na NMB
Akizungumza katika hafla ya kusaini makubaliano hayo iliyofanyika Serena Hotel jijini Dar es salaam mapema leo, Rais wa Yanga Injinia Hersi Said alisema Yanga inajivunia kuingia katika makubaliano hayo ambayo yatarahisisha kuwahudumia Wanachama kwenye Usajili na kutoa Kadi za Uanachama
"Ukijiunga kuwa Mwanachama wa Yanga, kupitia Benki ya NBC utapata kadi ya Uanachama na hapo hapo utapata huduma za kibenki, Lakini kubwa zaidi kadi ya NBC imeunganishwa na huduma za N CARD hivyo Mwanachama wetu atapata huduma ya kuingia Uwanjani pamoja na huduma za Usafiri"
"Niwaombe pia Benki ya NBC kutazama fursa nyingi zilizopo ndani ya Klabu yetu tuna Wanachama ndani na nje ya nchi na tunaamini Yanga ndio Klabu sahihi ya kufanya nayo kazi kwenye sekta ya michezo na nyie ni mashahidi, tangu mdhamini Ligi Kuu ya Tanzania Bara, Bingwa ni Yanga na niwahakikishie, kama mtaongeza Mkataba wa miaka 10 mbele, Bado Yanga atabaki kuwa Bingwa katika kipindi chote hiko," alisema Hersi



