Kocha Mkuu Yanga Miguel Gamondi amesema kikosi chake kiko tayari kwa mchezo wa robo fainali kombe la Shirikisho la CRDB dhidi ya Tabora United utakaopigwa kesho Jumatano katika uwanja wa Azam Complex
Gamondi amesema anatambua mchezo huo utakuwa mgumu kwani ni mechi ya mtoano lakini jambo jema ni kuwa watakuwa katika uwanja wa nyumbani na wachezaji wameonyesha kuwa tayari kwa ajili ya mchezo huo
"Ni mchezo wa robo fainali, tunafahamu hatua kama hizi mechi zinakuwa ngumu. Tunajua ubora wa mpinzani wetu hivyo tunapaswa kujiandaa vyema kwa ajili ya dakika 90"
"Ninajivunia kuwa na timu yenye umoja mkubwa namna hii kuanzia ndani na nje ya uwanja, wachezaji wangu wana njaa na kiu ya mafanikio, nimefurahishwa sana na mazoezi ya hapo jana," alisema Gamondi
Aidha Gamondi amedokeza kuwa kiungo mshambuliaji Pacome Zouzoua anaweza kupata nafasi ya kucheza katika mchezo huo baada ya kuridhishwa na maendeleo yake
"Ameanza kufanya mazoezi ya timu, naweza kusema yuko tayari kurejea uwanjani, nitamungalia baada ya mazoezi ya mwisho leo"
"Katika mchezo wa kesho, ninaweza kumpatia dakika 20..30.. kulingana na utayari wake, " alisema Gamondi



