Nyasi za Uwanja wa Benjamin Mkapa Dar es Salaam leo zitawaka moto katika mchezo wa kusaka heshima na nafasi ya kukata tiketi ya kucheza michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika msimu ujao
Azam FC leo wanakuwa nyumbani kuwakaribisha Simba, kwenye uwanja huo mchezo utakaochezwa saa 12:15 jioni huku timu zote zikihitaji matokeo katika mchezo huo
Simba wako nafasi ya tatu wakiwa na alama 53 ikiwa na mchezo mmoja mkononi huku wakiwa chini ya Azam kwa tofauti ya pointi nne huku Wanalambalamba hao wakishika nafasi ya pili nyuma ya vinara Yanga
Katika mchezo wa leo timu zote zinahitaji kupata matokeo chanya na endapo timu yoyote itaibuka na ushindi itajiweka kwenye mazingira mazuri ya kumaliza nafasi ya pili na kuendelea kutoa msukumo kwa Yanga kwenye kuwania ubingwa msimu huu
Kama Simba ikipoteza mechi ya leo itajiweka kwenye nafasi ngumu ya kushiriki Ligi ya Mabingwa Afrika kwa mara ya kwanza baada ya misimu zaidi ya mitano
Katika michezo 18 waliyokutana timu hizo, Simba imeshinda mara sita, imepoteza tatu na Azam FC imepata matokeo mara tatu na kupoteza sita, wote wametoka sare mara tisa
Kuelekea mchezo huo wa leo, Kaimu Kocha Mkuu wa Simba, Juma Mgunda alisema maandalizi ya mchezo yamekamilika na wapo tayari kushindana kupata matokeo mazuri
Alisema wanatambua Azam ni timu nzuri yenye kutoa ushindani lakini wamejipanga kufanya vizuri na kuondoka na pointi tatu
"Siku zote mchezo wa mpira kuna makosa hayakwepeki, kikubwa ni kuyafanyia kazi katika uwanja wa mazoezi, mechi iliyopita tulifanya makosa naamini tumesahihisha na kuyapunguza tayari kwa mchezo wa leo"
"Soka ni mchezo wa wazi hakuna kuficha, tunaingia uwanjani kusaka pointi tatu ambazo ni muhimu sana, leo tutaendelea kumkosa Chama (Clatous) ambaye ni majeruhi na anatumikia adhabu, Miquison, Ntibazonkiza, Onana wote ni majeruhi pia, lakini hiyo sio tatizo kwa kuwa wachezaji waliopo ni waajiriwa wa Simba atakayepewa jezi atatakiwa kutumikia timu na kuhakikisha tunapata ushindi," alisema Mgunda
Kocha wa Azam FC, Bruno Ferry alisema mara ya mwisho walikutana na Simba katika mashindano ya Muungano na kupoteza, hivyo wataingia uwanjani kwa tahadhari wakitaka pointi tatu
Alisema wamejipanga vizuri, wachezaji wapo tayari kwa ajili ya mchezo wa leo na kusaka pointi tatu muhimu mbele ya wapinzani wao kwa ajili ya kufikia malengo yao
"Ni mechi ya ushindani mkubwa, Simba wako vizuri, tumefanya maandalizi mazuri na wachezaji wapo tayari kwa mchezo, naomba waamuzi kuwa waungwana kwa sababu maamuzi mengi yamekuwa yakiharibiwa, wawe makini ili uwe mchezo wa haki," alisema Bruno



